Diamond Kufanya Collabo na Wiz Khalifa

[Picha: Diamond Platnumz Instagram]

Mwandishi: Charles Maganga

Pata Habari za Muziki na Mixtapes Bure Kwenye Telegram

Hata baada ya kukosa tuzo ya BET mbele ya Burna Boy, Diamond Platnumz ameendelea kuonesha nia yake ya kustawisha muziki wa Tanzania kwenda kimataifa.

Hii ni baada ya kuchapisha picha katika akaunti yake ya Instagram ikimuonesha akiwa na msanii Wiz khalifa kutokea nchini Marekani ambapo amekwenda kwa ajili ya maandalizi ya mwisho kabisa ya albamu yake ambayo inatarajiwa kuwafikia mashabiki zake hivi karibuni.

Soma Pia: Busta Rhymes Amsifu Diamond, Amtaja Kuwa Michael Jackson wa Afrika

Chapisho hilo kutoka kwa Diamond lilisindikizwa na ujumbe : " Wasafi × Taylor Gang" huku akiweka tagi kwa Wiz Khalifa ambaye aliburudisha wapenda muziki duniani kote mwaka wa 2015 baada ya kutoa wimbo wake uitwao ‘See You Again’ ambao umetazamwa takribani mara Bilioni tano kwenye mtandao wa YouTube.

Kando na Wiz Khalifa, Siku nne zilizopita Diamond aliweka video kwenye mtandao wa Instagram akiwa studio na msanii Busta Rhymes, kisha siku chache baadae alionekana kwenye picha na mtayarishaji wa muziki Swizz Beats ambaye ni mume wa msanii Alicia Keys.

Soma Pia: Nyimbo Mpya: Ngoma Mpya Zilioachiwa na Diamond, Rayvanny, Harmonize na Alikiba Wiki Hii

Diamond Platnumz pia alitangaza kuwa rapa Swae Lee atahusika pia kwenye albamu yake. Hili sio jambo geni kwa Diamond Platnumz kufanya kazi na wasanii kutokea nchini Marekani, kwani kwenye albamu yake, ‘A boy from Tandale’ iliyotoka Machi mwaka 2018 pia alishirikisha wasanii wakubwa kutokea nchini humo.

Alianza kufanya kazi na Shaffer Smith almaarufu kama Neyo kwenye wimbo wa ‘Marry You’ ambao ulitoka Januari 2017 huku video ya wimbo huo ikiwa imetazamwa mara milioni 51 mpaka sasa.

Miezi 11 baadae akatoa wimbo na rapa Rick Ross uitwao ‘Wakawaka’ kisha Machi 2018 akashirikiana na Omarion wa kundi la B2k kwenye wimbo wa kwenye ‘African Beauty’ ambao mpaka sasa video ya wimbo huu imetazamwa mara milioni 61 kwenye mtandao wa YouTube.

Kwa sasa, Diamond platnumz anatamba na wimbo wake uliotayarishwa na S2kizzy uitwao "Kamata" na mengi makubwa yanatarajiwa kuonekana kutoka kwa staa huyo.

Leave your comment