Babu Tale Amsifu Nandy Baada ya Tamasha Yake ‘Nandy Festival’ Kufanya Vyema

[Picha: Nandy Instagram]

Mwandishi: Charles Maganga

Pata Habari za Muziki na Mixtapes Bure Kwenye Telegram

Meneja wa Diamond Platnumz Khamis Taletale almaarufu kama Babu Tale amempongeza mwanamuziki Faustina Mfinanga aka Nandy kutokana na tamasha lake la Nandy Festival kufanya vizuri.

Babu Tale amempongeza Nandy kwa ujasiri wake wa kuweza kufanya tamasha hilo ambalo linahusisha wasanii tofauti tofauti wa nchini Tanzania.

Read Also: Tamasha la Nandy Festival Lapata Mafanikio Makubwa Kigoma

"Kwanza nimpongeze Nandy, unajua ukiona msanii wa kike anaweza kupull crowd kubwa unampa heshima kubwa sana. Nandy anafanya vizuri sana na ni moja kati ya wasanii wanaofanya vizuri sana Tanzania safari hii. Apewe heshima yake,” Babu Tale alinena.

Nandy Festival inategemewa kuzunguka mikoa mbalimbali hapa Tanzania ambapo mpaka sasa tamasha hilo lishafanyika Kigoma pamoja na Mwanza na wikiendi hii tamasha hili linategemewa kurindima mji mkuu wa Tanzania, Dodoma.

Soma Pia: Nyimbo Mpya: Nandy Azungumzia Mahusiano ya Rayvanny, Harmonize na Jux Kwenye ‘New Couple’

Kando na kumpa pongezi, Babu Tale alithibitisha kuwepo kwenye tamasha hilo litakalofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri.

"Tumepata bahati anakuja (Nandy) anakuja Dodoma wakati sisi tupo Dodoma nitakuwa mbele kumpokea Nandy. Nandy karibu Dodoma uje uienjoy,” Babu Tale alisema.

Jukwaa la Nandy Festival Dodoma linategemewa kupamba moto na kuwa na mvuto wa aina yake baada ya Nandy kutangaza kuwa mwanamuziki kutokea nchini Kenya Tanasha Donna atashiriki katika tamasha hilo, hiyo inamfanya Tanasha kuweka rekodi ya kuwa msanii wa kwanza nje ya Tanzania kushiriki kwenye tamasha hilo.

Mbali na Tanasha, wasanii wengine ambao washathibitisha kuwepo Dodoma ni Rosa Ree pamoja na Professor Jay na kulingana na manager wa Nandy amesema mpaka ifikapo Jumamosi wasanii wote washiriki watakuwa wamewekwa wazi.

Nandy hivi karibuni aliachia EP yake iitwayo Taste EP yenye nyimbo nne ili kuweza kunogesha tamasha hilo.

Leave your comment