Kama alivyotu penda

Mungu Anakujali Kwelikweli
NI JAMBO la kawaida kumlilia Mungu atusaidie tunapokuwa katika shida. Hiyo ni kwa sababu yeye “ni mkuu na mwenye nguvu nyingi; uelewaji wake hauwezi kusimuliwa.” (Zaburi 147:5) Yeye hasa ndiye anayeweza kutusaidia kukabiliana na matatizo yetu. Pia, Biblia hutualika ‘tumimine moyo wetu’ mbele zake. (Zaburi 62:8) Hivyo, kwa nini watu wengi sana hufikiri kwamba Mungu hajibu sala zao? Je, hiyo inamaanisha kwamba yeye hajali?
Badala ya kumlaumu Mungu haraka-haraka kwa kuonekana kama hajali, kumbuka wakati ulipokuwa mtoto. Wazazi wako walipokataa kukutimizia kila jambo ulilotaka, je, uliwahi kuwashutumu kwamba hawakupendi? Watoto wengi hufanya hivyo. Hata hivyo, ulipokua ukawa mtu mzima, ulitambua kwamba upendo huonyeshwa katika njia nyingi, na kwamba kumwonyesha mtoto upendo hakumaanishi kumtimizia kila jambo analotaka.
Vivyo hivyo, haimaanishi kwamba Yehova anatupuuza ikiwa sikuzote hatajibu sala zetu kupatana na matarajio yetu. Ukweli ni kwamba Mungu huonyesha kwa njia nyingi kwamba anatujali sisi sote.
“Kwake Tuna Uhai”
Kwanza kabisa, sisi “tuna uhai na tunaenda na kuwako” kwa sababu ya Mungu. (Matendo 17:28) Bila shaka, kwa kutupa uhai, Mungu ameonyesha kwamba anatujali!
Pia, Yehova hutuandalia mahitaji yetu ili tuendelee kuwa hai. Tunasoma: “Anafanya majani mabichi yachipuke kwa ajili ya wanyama, na mimea ili itumikie wanadamu, ili chakula kitokezwe duniani.” (Zaburi 104:14) Kwa kweli, Muumba wetu hatuandalii tu mahitaji ya msingi ya maisha. Kwa ukarimu, yeye hutupa “mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo [yetu] kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17.
Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza, ‘Ikiwa Mungu anatupenda sana hivyo, kwa nini yeye huruhusu tuteseke?’ Je, unajua jibu la swali hilo?
Je, Mungu Ndiye Husababisha Matatizo Yetu?
Mwanadamu ndiye husababisha mengi ya matatizo yanayompata. Kwa mfano, tunajua vizuri sana hatari zinazotokana na vitendo fulani. Na bado, watu hufanya uasherati, hutumia vibaya pombe na dawa nyingine, hutumia tumbaku, hushiriki katika michezo hatari, kuendesha gari kwa kasi, na kadhalika. Tumlaumu nani ikiwa mtu atateseka kwa sababu ya mazoea hayo hatari? Mungu au yule anayetenda kipumbavu? Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linasema: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.
Pia, mara nyingi wanadamu huumizana. Taifa linapotangaza vita, bila shaka, Mungu hawezi kulaumiwa kwa mateso yanayotokea. Mhalifu anapomshambulia raia mwenzake, je, tumlaumu Mungu kwa majeraha yoyote yanayotokea au kifo? La! Je, tumlaumu Mungu wakati mtawala wa kimabavu anapokandamiza, kutesa, na kuwaua watu anaotawala? Hilo halingekuwa jambo la akili.—Mhubiri 8:9.
Lakini namna gani mamilioni ya wale wanaoishi maisha ya ufukara au wana njaa? Je, tumlaumu Mungu? La, kwa kuwa dunia yetu huzalisha chakula cha kutosha kulisha kila mtu. (Zaburi 10:2, 3; 145:16) Kuna njaa na umaskini mwingi kwa sababu vitu ambavyo Mungu ametupatia havigawanywi kwa usawa. Na tatizo hilo haliwezi kutatuliwa kwa sababu ya ubinafsi wa mwanadamu.
Sababu ya Msingi
Lakini je, tumlaumu nani mtu anaposhikwa na ugonjwa au anapokufa kwa sababu ya uzee? Je, ungeshangaa kujua kwamba hatupaswi kumlaumu Mungu kwa mambo hayo? Mungu hakumuumba mwanadamu awe akizeeka na kufa.
Wakati wenzi wa kwanza, Adamu na Hawa, walipowekwa katika bustani ya Edeni, Yehova aliwapa taraja la kuishi milele katika paradiso duniani. Hata hivyo, ni wazi kwamba alitaka dunia ikaliwe na watu ambao wangethamini urithi wao. Hivyo, matarajio ya uhai wao wa wakati ujao yangetegemea sharti fulani. Adamu na Hawa wangeishi katika Paradiso ikiwa tu wangeendelea kumtii Muumba wao mwenye upendo.—Mwanzo 2:17; 3:2, 3, 17-23.
Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa waliasi. Hawa aliamua kumsikiliza Shetani Ibilisi. Shetani alimdanganya na hivyo akaonyesha kwamba Mungu alikuwa akimnyima Hawa kitu fulani kizuri. Hivyo, akaanza kujitegemea na kujaribu ‘kuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ Adamu aliungana naye katika uasi huo.—Mwanzo 3:5, 6.
Kwa kutenda dhambi hiyo, Adamu na Hawa walionyesha kwamba hawastahili kuishi milele. Walipatwa na matokeo mabaya ya dhambi. Nguvu zao zilipungua, na mwishowe wakafa. (Mwanzo 5:5) Hata hivyo, uasi wao ulikuwa na matokeo mabaya zaidi. Tungali tunateseka kutokana na dhambi ya Adamu na Hawa. Mtume Paulo aliandika: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Naam, kwa sababu ya uasi wa Adamu na Hawa, dhambi na kifo vilienea kati ya wanadamu wote kama ugonjwa wenye kuua.
Uthibitisho Wenye Nguvu Zaidi Kwamba Mungu Anajali
Je, hiyo inamaanisha kwamba wanadamu walipatwa na madhara ya kudumu? La, na sasa tunaona uthibitisho wenye nguvu zaidi kwamba Mungu anatujali. Kwa bei

Leave your comment