Nandy Atambulisha Lebo Yake Mpya "African Princess"

[Picha: Instagram]

Mwandishi: Charles Maganga

Pata Habari za Muziki na Mixtapes Kwenye Telegram

Mwanamuziki nguli kutoka Tanzania, Faustina Charles Mfinanga maarufu kama Nandy amegonga vichwa vya habari hivi karibuni baada ya kutangaza kuanzisha lebo yake mwenyewe ya muziki.

Nandy ambaye alipata umaarufu mkubwa Tanzania mwaka 2016 baada ya kuachia Nagusa Nagusa pindi akiwa chini ya THT ametoa taarifa hizo hivi karibuni. Nandy kwa muda mrefu sasa amekuwa ni msanii huru ambaye hajafungamana na lebo yoyote huku mara nyingi akionekana akifanya kazi kwa ukaribu zaidi na kampuni ya  EmPawa ya Mr Eazi.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Nandy ametangaza kwamba lebo yake itaitwa The African Princess na kwamba lebo hiyo itakuwa inasimamia hasa wasanii wa kike tu ili kuweza kuziba pengo kwenye muziki wa Tanzania kwani wasanii wa kike bado ni wachache.

"Ninayo furaha kubwa kuileta kwenu Rasmi THE AFRICAN PRINCESS LEBEL...! 2023 lebel ambayo itahusisha wanawake tu! Kama tunavo ona industry ya watoto wa kike ni chache sana na uthubutu umekuwa ni mdogo so tunaimani na kuomba the African princess lebel itaongeza wingi wa vipaji vya watoto wa kike waliopo mtaaani wenye ndoto kubwa ya kuwa wanamziki!!" aliandika Nandy kwenye ukurasa wake wa Instagram.

Kando na Nandy wasanii wengine wa kike kutoka Tanzania ambao wameshawahi kufungua lebo zao ni pamoja na Vanessa Mdee ambaye miaka kadhaa nyuma alifungua Mdee Music ambayo ilisimamia kazi zake yeye, Mimi Mars pamoja na Brian Simba ambaye kwa sasa ameshaondoka kwenye lebo hiyo.

Leave your comment