Diamond ‘Gimmie’, Lulu Diva ‘Kawaida’ na Nyimbo Zingine Mpya Zilizoachiwa Bongo Wiki Hii
18 October 2021
[Picha: YouTube]
Mwandishi: Charles Maganga
Pata Habari za Muziki na Mixtapes Bure Kwenye Telegram
Kama unapenda muziki mzuri, basi bila shaka wiki hii imekuwa ni njema sana kwako kwani wasanii mbalimbali kutokea Tanzania wameachia ngoma mpya nzuri nzuri. Makala hii imelenga kukupitisha kwenye zile ngoma mpya ambazo zimedondoka kwenye soko la muziki nchini Tanzania kwa wiki hii:
Soma Pia: Sababu Tano Kuu Zinazoeleza Mbona Tasnia ya Muziki ya Tanzania Inahitaji Tuzo Za Kinyumbani
Gimmie - Diamond Platnumz ft Rema
Mwanamuziki Diamond Platnumz ameachia ngoma yake ya nne kwa mwaka huu ya kuitwa ‘Gimmie’ ambayo ameshirikiana na Rema kutokea Nigeria. Tangu iingie sokoni, ‘Gimmie’ imekuwa ni tishio na wimbo mkubwa sana hapa Afrika Mashariki kutokana na mdundo wake.
Maelekezo Chapter 2 - Moni Centrozone ft Rapcha & Maarifa Rapa
Moni ameendelea kuonesha cheche zake kwenye muziki wa Hip-hop baada ya kuachia ngoma yake ya ‘Maelekezo Chapter 2’. Kwenye ngoma hii, Moni anagusia masuala mbalimbali kama ushindani kwenye muziki, watu wanaopenda starehe, urafiki wa kinafiki na mambo mengi.
Unaota - Baddest 47
Baddest 47 ameendelea kujitengenezea historia ya aina yake kwenye muziki wa Bongo Fleva na ngoma yake mpya ya kuitwa ‘Unaota’ imethibitisha hilo. Kwenye ngoma hii, Baddest kama kawaida yake anagusia masuala tofauti tofauti ya kimaisha huku akitumia neno ‘Unaota’ kufikisha ujumbe wake.
Kawaida - Lulu Diva
Kama unatafuta ngoma ambayo itakufanya ucheze, ucheke na kufurahi kwa wakati mmoja, basi wiki hii Lulu Diva amekidhi haja yako baada ya kuachia ngoma yake mpya ‘Kawaida’. ‘Kawaida’ imeandikwa na ‘Whozu’ na mtayarishaji wa muziki S2kizzy Ndiye amehusika kupika mdundo wa ngoma hiyo.
Kama Unae - Rapcha ft Kid Golden
Rapa kutokea Tanzania Rapcha ameachia rasmi ngoma na video ya ‘Kama Unae’ ambayo humu ndani anamsifia mpenzi wake. Anamwambia kama ataweza sio vibaya akimuweka hadharani kwa watu kupitia mitandao ya kijamii. Kufikia sasa ngoma hii imeshatazamwa mara elfu sitini na nne kwenye mtandao wa YouTube.
Leave your comment