TANZANIA: Baada ya Mzee Yusuph kuacha muziki, aenda kuhij Makkah

 

 

 

Mfalme wa muziki wa taarabu nchini, Mzee Yusuf, ameondoka nchini jana Agosti 31, 2016 kwenda kuhij Makkah ili kutimiza moja kati ya nguzo kuu za dini yake ya Kiislam.

Mzee kabla hajakwea pipa, eNewz ilifanikiwa kufanya mahojiano naye ambapo amesema hatua ya kwenda kuhiji aliipanga iwe mwaka 2018 lakini kwa vile ana nguvu na uwezo ameona aende mwaka huu.

“Nilipanga kwenda kuhiji mwaka 2018 lakini Allah kanifanya niamue tu kwenda mwaka huu kwa kuwa nimeona nina uwezo wa kwenda na kutimiza nguzo hii muhimu katika dini ya kiislamu na namuomba Mungu anijalie uzima nirudi salama ili niweze kwenda tena kwa mara nyingine” Mzee Yusuf aliiambia eNewz.

Akiwa amemsindikiza Mzee uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam, baba mzazi wa mzee Yusuph amesema mwanaye kuacha muziki ni jambo zuri hasa kuamua kumtumikia Mungu na kusema anazidi kumuombea mema.

“Mzee kuacha muziki ni jambo la kheri pia kitendo cha kuamua kuacha kuimba na kuendelea kumtumikia Allah ni vizuri zaidi hivyo namuombea Mungu aendelee na moyo huo huo” Aliongea baba mzazi wa msanii huyo.

Hata hivyo eNewz iliendelea kupiga story na mke wake ambaye pia ni muimbaji wa Band ya Jahazi, Laila Rashid ambaye alisema “Mimi binafsi namuombea Mzee kila la kheri katika maamuzi aliyoyafanya na Mungu ampe nguvu katika kila jambo analopanga kulifanya kwa sasa.

Pia Laila alimalizia kwa kusema sababu iliyopelekea kuachiwa albam ambayo ilitungwa wakati mzee akiwepo na kusema wameiachia kwa kuwa ilirekodiwa kipindi mzee akiwa kwenye muziki hivyo ilikuwa lazima albam hiyo itoke na kusema wakati ukifika naye atafuata nyayo za mzee kuacha muziki.

 

Mzee Yusuph na mkewe Leila Rashid

Pakua app ya Mdundo sasa: smarturl.it/mdundo_ig_play_tz

Leave your comment