Meja Kunta Atangaza Ujio wa EP Yake Mpya

[Picha: Tabell East Africa ]

Mwandishi: Charles Maganga

Pata Habari za Muziki na Mixtapes Bure Kwenye Telegram

Mwanamuziki wa Singeli kutokea Tanzania Meja Kunta ametangaza ujio wa EP yake mpya ambayo anatarajiwa kuachiwa hivi karibuni.

Meja Kunta ambaye kwa sasa amegusa hisia za mashabiki wa soka nchini Tanzania baada ya kuachia wimbo wake wa ‘Simba’ ametoa taarifa hiyo akiwa kwemye mahojiano kwenye kipindi cha E Newz.

Soma Pia: Nyimbo Mpya: Meja Kunta Aachia Wimbo Mpya ‘Simba’

Katika mahojiano hayo Meja Kunta alisema kuwa hivi karibuni ataachia EP hiyo ambayo hajashirikisha msanii yeyote.

Uamuzi wa kutoshirikisha msanii yeyote kwenye EP yake unakuja kwenye kipindi ambacho kumekuwa na gumzo kuwa Meja Kunta anabebwa sana na collabo kuliko nyimbo ambazo anafanya mwenyewe.

Meja Kunta ametumia mahojiano hayo kusema kuwa habebwi na pia kuongeza kuwa ngoma zake zote huandika mwenyewe.

Soma Pia: Meja Kunta Aitaja Singeli Kuwa Muziki Bora Zaidi Tanzania

"Mwenyezi Mungu amenijalia huwa ngoma zangu naandika mimi mwenyewe hata collabo nyingi unazoziona nimeandika mimi mwenyewe nyingi sana," alizungumza Meja Kunta.

Kama Meja Kunta ataachia EP hiyo mwaka huu basi atakuwa ni msanii wa pili wa singeli ambaye ameachia EP baada ya Man Fongo kuachia EP yake ya ‘Ndio Basi Tena’ mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu.

Meja Kunta ni mojawapo ya wasanii wa Singeli wanaotamba sana nchini Tanzania na muziki wake ulipata mwitikio mkubwa zaidi baada ya kushirikiana na Lavalava kwenye ngoma ya ‘Wanga’.

Leave your comment